06/11/2009 14.55.25


Askofu mteule Festo Ngowo wa KKKT dayosisi ya Dodoma kusimikwa rasmi jumapili ijayo!


|

Askofu Mteule wa Kanisa la Kiinjili la kilutheri Tanzania, KKKT., Dayosisi ya Dodoma Mhashamu Festo Ngowo anatarajiwa kusimikwa rasmi siku ya jumapili tarehe 8 Novemba, 2009 kushika nafasi ya Askofu Peter Mwamasika aliyestaafu shughuli za kichungaji baada ya kuitumia Dayosisi ya Dodoma kwa kipindi cha miaka ishirini na moja. Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na kaimu katibu mkuu wa kanisa la KKKT Dayosisi ya Dodoma, mchungaji Victoria Ntega anasema kwamba, ibada kwa ajili ya kusimikwa askofu mteule Festo Ngowo itaanza majira ya saa 3 asubuhi kwenye kanisa kuu la KKKT, mjini Dodoma na itaongozwa na mkuu wa kanisa hilo Askofu mkuu Alex Malasusa. Kwa mujibu wa taarifa hiyo ibada hiyo itahudhuriwa na viongozi mbalimbali wa dini na serikali akiwemo Waziri Mkuu wa Tanzania Mizengo Pinda na Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania, Askofu Yuda Thadei Ruwaich. Aidha wageni wengine walioalikwa wametoka katika nchi za Marekani, Ujerumani, Sweeden na Maaskofu kutoka katika makanisa ya mkoa wa Dodoma na mikoa ya jirani. Katika Ibada hiyo ya kumsimika askofu Ngowo pia kutakuwepo na tukio la kutunukiwa shahada ya heshima kwa mkuu wa kanisa hilo Askofu mkuu Alex Malasusa.
|