07/11/2009 11.50.00


Upendo kwa Kristo na Kanisa lake ujidhihirishe katika huduma kwa maskini


|

Kardinali Tarcisio Bertone, katibu mkuu wa Vatican siku ya jumamosi, tarehe 7 Novemba, 2009 ameadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwa ajili ya wakuu wa mashirika ya kitawa nchini Italia waliokuwa wanahudhuria mkutano wao wa arobaini na tisa, maadhimisho ambayo yamekwenda sambamba na Jubilee ya miaka mia moja na hamsini, tangu Shirika la Wasalesiani wa Don Bosco lilipoanzishwa.
Wakuu wa Mashirika ya kitawa na kazi za kitume kwa muda wa wiki nzima wamekuwa wakitafakari juu ya umaskini na ushirikiano wa mafao ya wengi katika ulimwengu wa utandawazi, kama njia ya kuonesha ushuhuda wa maisha ya kuwekwa wakfu.
Kardinali Bertone aliwapatia wakuu hao wa mashirika salam na matashi mema kutoka kwa Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita anayewaalika kuendelea kujitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya Kristo na Kanisa lake, ili kutangaza Habari Njema ya Wokovu. Amewaasa watawa kutumia vyema mali ya dunia kwa ajili ya ujenzi wa ufalme wa Mungu, unaojidhihirisha katika kazi za kitume mintarafu wito wa maisha ya kitawa.
Msingi wa maisha haya anasema Kardinali Bertone, ni Kristo mwenyewe, kwani hata katika umaskini wa mtu binafsi, lakini akiwa amejitajirisha kwa Kristo anakuwa na uwezo wa kujenga maisha ya kidugu katika Jumuiya. Ni changamoto ya kuwa wakweli na wa wazi, ili kung'oa ndazo za wasi wasi na woga usiokuwa na msingi, unaoweza kuathiri maisha ya kijumuiya.
Anawaalika watawa kuendelea kuonesha upendo, furaha na nguvu hali wakijitahidi kujinyima kwa ajili ya mafao ya wengine pamoja na kutumia vyema karama walizokirimiwa na Mwenyezi Mungu kwa ajili ya ustawi wa mashirika yao kama kielelezo cha shukrani kwa Mwenyezi Mungu. Umaskini na umoja kwa mafao ya wengi katika ulimwengu wa utandawazi ni ushuhuda amini kwa maisha ya kitawa.
Kardinali Bertone ametolea mfano wa ushuhuda wa maisha ya kitawa uliofanywa na Mtakatifu Don Bosco anayeendelea kutoa changamoto kwa Wasalesiani wa Don Bosco, ili kuendeleza majiundo kwa vijana, ili hatimaye waweze kuwa ni wakristo wema na wananchi waaminifu.
Utume wa Mtakatifu Bosco na wasaidizi wake wa kwanza haukuwa ni lelemama, bali iliwabidi kujifunga kibwebwe, kwa uvumilivu, upendo na uhusiano binafsi kati yao, ujasiri pamoja na matumaini ndani ya Kanisa, chini ya uongozi wa Khalifa wa Mtakatifu Petro.
Don Bosco na wafuasi wake walijitahidi kujifunga kibwebwe kwa ajili ya kutangaza Habari Njema ya wokovu, kwa kuwajenga matumaini vijana kwamba Mwenyezi Mungu yupo na ni mwingi wa huruma na mapendo. Daima Don Bosco aliendelea kumjifunza Kristo kwa njia ya shule ya Bikira Maria. Mipango yake ya kichungani ilipania kupambana na uwepo wa dhambi pamoja na kueneza Ibada kwa Bikira Maria, inayopaswa kumwilishwa katika shughuli za kiuchumi, kijamii, kichungaji na kielimu.
Mama Kanisa anaendelea kutoa changamoto kwa watawa kuwa karibu na vijana ili kuwasaidia katika hija ya maisha yao kama alivyofanya Mtakatifu Don Bosco. Utume kwa vijana unaweza kufanyika kwa kukazia zaidi upendo, maisha ya kisakramenti, ili kuwasaidia vijana kujenga uhusiano wa karibu na Kristo; Utangazaji wa Neno la Mungu, ambao kwa Don Bosco ulifumbata mikakati ya elimu kwa vijana.
Kardinali Tarcisio Bertone anawakumbusha wakuu wa mashirika kwamba, upendo kwa Kristo na Kanisa lake ujidhihirishe katika huduma kwa watu maskini katika mahitaji yao ya kiroho na kimwili
|