07/11/2009 10.38.06


Benedikto XVI asema: michezo ina nafasi ya pekee katika maisha na majiundo ya vijana kiroho na kimwili


|

Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita katika ujumbe wake aliomwandikia Kardinali Stanslaw Rylko, Rais wa Baraza la Kipapa kwa ajili ya walei pamoja na washiriki wote wa semina inayojadili kuhusu michezo, elimu na imani katika mwelekeo mpya wa shughuli za michezo anasema, michezo ina nafasi ya pekee katika maisha ya vijana, majiundo ya mtu mzima na matumizi sahihi ya muda.
Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican anasema Baba Mtakatifu unatambua dhamana na nafasi ya michezo katika majiundo ya mtu kimaadili, kiutu na kikristo katika ulimwengu wa kizazi kipya. Ni fursa ya kuboresha mwili wa mtu na shule makini ya tunu msingi za kiutu, kibinadamu na katika maisha ya kiroho. Michezo ikitumiwa vyema kama sehemu ya majiundo ya mtu mzima inakuwa ni fursa kwa viongozi wa Kanisa kuwasaidia vijana katika majiundo yao.
Baba Mtakatifu anasema, Kanisa litaendelea kuwekeza katika michezo kwa vijana, likiwasaidia kujenga tunu bora zinazoibuliwa katika michezo kama vile ushindani, ujasiri na ari ya kufikia malengo yaliyowekwa; hali wakijitahidi kukwepa mambo yote yanayoweza kuharibu nafasi ya michezo katika maisha ya vijana.
Vijana wanapaswa kutumia vyema nafasi ya michezo, ili kuendeleza vipaji na karama zao, sanjari na tunu za kiutu na kikristo ili kufikia ukomavu kamili. Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita analipongeza Baraza la Kipapa kwa ajili ya walei kwa kuandaa semina kama hii, ili kutoa mwelekeo wa Kanisa katika masuala ya kichezo. Michezo ni fursa nzuri ya shughuli za kitume kwa vijana.
|